Katika juhudi za kuhakikisha wananchi wanapata uelewa wa haki zao, timu ya Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi mkoani Rukwa imetembelea Kijiji cha King’ombe, Kata ya Kala, kupitia kampeni ya msaada wa kisheria inayotekelezwa chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.
Kupitia kampeni hii, wananchi wamepewa elimu kuhusu masuala mbalimbali ya kisheria yanayohusu ardhi, mirathi, ndoa, ukatili wa kijinsia, na haki za binadamu. Lengo kuu la kampeni hii ni kuwawezesha wananchi kutambua na kutetea haki zao kwa mujibu wa sheria, pamoja na kujenga jamii yenye usawa na haki kwa wote.
Kwa kutoa elimu ya kisheria, serikali inalenga kupunguza migogoro inayotokana na ukosefu wa uelewa wa sheria, huku ikihimiza utatuzi wa migogoro kwa njia ya amani. Wananchi wa King’ombe wamepongeza juhudi hizi na kueleza kuwa zitasaidia sana katika kuimarisha ustawi wa jamii na maendeleo yao kwa ujumla.